TIKITAKA ZA MENEJIMENTI YA ATC
Baada ya Menejimenti ya Chuo cha ufundi Arusha kutumia Bodi ya Uongozi wa Chuo kufanikisha mambo yake, sasa imekumbuka kwamba kuna Baraza la Wafanyakazi. Baraza la Wafanyakazi wa Chuo limekuwepo kama alama tu ya Baraza lakini kwa Menejimenti ya Chuo, Baraza la wafanyakazi si lolote si chochote.
Baada ya kutelekeza Baraza la Wafanyakazi na shughuli zake kwa takribani miaka miwili, hivi sasa Menejimenti ya chuo umekumbuka kwamba Baraza lipo na linatakiwa kushauri Menejimenti ya chuo kuhusu mambo mbalimbali kwa mujibu wa sheria kwa manufaa ya Chuo na wafanyakazi.
Inaaminika kwamba kwa kuwa Mwenyekiti wa Bodi ya Uongozi wa chuo alimaliza muda wake na baada ya Bodi ya uongozi wa Chuo kulalamikiwa kwa mambo mengi, pengine sasa ni zamu ya Baraza la Wafanyakazi
Hakuna anayefahamu kwamba kwa kipindi kirefu namna hiyo Menejimenti ya Chuo ilikuwa inapata wapi ushauri wa mambo mbalimbali yaliyofanywa na Menejimenti bila Baraza la Wafanyakazi. Kwa baraza kukaa muda mrefu bila kikao ina maana hakutakuwa na muhtasari wa kikao kilichotangulia wala yatokanayo na kikao hicho kwenye ajenda zake, maana ilishasahaulika na hakuna anayekumbuka kilichojadiliwa katika kikao kilichopita.
Vikao vya Baraza la wafanyakazi vilipigwa chenga kwa kuwa pengine siri za mapato na matumizi ya chuo zingejulikana kwa wafanyakazi. Pengine kitendo cha Mheshimiwa Rais kuelekeza kwamba mapato yote ya Taasisi za umma yapelekwe BOT ni pigo na sasa Menejimenti ya chuo haina cha kuficha tena. Hivyo Baraza ni ruksa sasa kukaa vikao vyake kuishauri Menejimenti iliyokataa ushauri wa Baraza siku za nyuma.
Haifahamiki ni kitu gani kimeisukuma Menejimenti ya Chuo kutaka kuwe na kikao cha Baraza la Wafanyakazi wakati huu ambapo Menejimenti hiyo ikiwa na Tuhuma lukuki za Ufisadi na Matumizi mabaya ya madaraka.
Re: TIKITAKA ZA MENEJIMENTI YA ATC
Ni muda takriban wa miaka miwili ambako kulikuwa hakuna vikao vya baraza la wafanyakazi. Je ni nani walikuwa wanapanga mapato na matumizi ya Chuo? Je Bodi ya Chuo ilikuwa ikikaa inajadili nini? Au kujadili hoja zinazotoka wapi? Labda kwa kuwa hakukuwa na chombo chochote kilichokuwa kinapanga mapato na matumizi ya taasisi hii ndo maana mambo yakaenda vibaya. Kama kungekuwapo na vikao vya baraza la wafanyakazi inavyotakiwa huenda leo kungekuwa shwari hapo hata harufu inayozungumzwa ya ufisadi isingekuwapo. Nataadharisha, kuitishwa kikao cha baraza muda huu ambao kuna tuhuma nyingi za ufisadi chuoni, inatakiwa umakini kusijekuwa kuna hoja zinatakiwa kuchomekwa hapo ambazo ziko kwenye chokochoko hizi za ufisadi zilizojitokeza ili ionekane yalikuwakuwa ni mambo yaliyopitishwa na baraza la wafanyakazi.